Sunday 24 December 2017

Watu 22 wahofiwa Kufa Maji ziwa Tanganyika baada ya boti kugongana

Maafisa nchini Tanzania wanasema karibu watu ishirini na wawili wanahofiwa kufa maji baada ya boti kugongana katika ziwa Tanganyika mapema leo asubuhi.
Mashua moja iliyokuwa imebeba takriban watu mia moja na arubaini waliyokuwa safarini kwa shughuli ya kidini iligongana na boti iliyokuwa na watu sitini na watano.
Usafiri wa nyakati za usiku umepigwa marufuku katika ziwa Tanganyika.
Kwa mujibu wa Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Sweetbert Njewike, wanaendelea kuwatafuta watu ambao hawajaonekana waliokuwa wakisafiri na vyombo hivyo.

Alisema shughuli za uokoaji zinafanywa kwa pamoja na vikosi vya Polisi, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na wananchi.
KUlingana na gazeti la mwananchi nchini humo mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mwanamvua Mrindoko amesema kuwa uchunguzi wa awali unaonyesha kwamba kulikuwa na dosari zilizosababisha ajali hiyo.
Alizitaja dosari hizo kuwa ukosefu wa vifaa vya uokoaji, vya kuzima moto mbali na boti kufanya safari za usiku.

0 comments: