Sunday 17 December 2017

KIMATAIFA: UN kupigia kura mswada kuhusu Jerusalem.

 Balozi wa Misri katika Umoja wa mataifa Abdellatif Aboulatta.

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linatafakari kupitisha mswada unaosema mabadiliko yoyote ya hadhi ya  mji wa Jerusalem hayatakuwa na athari kisheria na yanapaswa kubadilishwa. 
Misri imesambaza mswada  huo Jumamosi (16.12.2017), na wanadiplomasia  wamesema baraza  huenda  likapiga kura kuhusiana  na  mapendekezo  hayo mapema  hata  Jumatatu.
Akijitoa  katika  mwelekeo wa  kimataifa , rais  wa  Marekani Donald Trump  mwezi huu alitangaza  kwamba  atautambua  mji  wa  Jerusalem  katika  mji  mkuu  wa  Israel  na kuhamishia  ubalozi  wa  Marekani  katika  mji  huo  kutoka  Tel Aviv, hatua  hiyo  imezusha maandamano  na  shutuma  kali.
Mswada  huo  wa  azimio  uliopatikana  na  shirika  la  habari  la  AFP  unasisitiza  kwamba Jerusalem  ni  suala , "ambalo  linaamuliwa  kupitia  majadiliano"  na  kueleza "masikitiko makubwa  katika  uamuzi  wa  hivi  karibuni  kuhusiana  na  hadhi  ya  mji  wa  Jerusalem," bila kutaja  moja  kwa  moja  uamuzi  wa  rais Trump.
"Uamuzi  wowote  na  hatua  ambazo  zitaonekana  kubadilisha  hadhi, hali  na  jamii  iliyopo katika  mji  huo  mtakatifu  wa  Jerusalem  havitakuwa  na  athari  ya  kisheria, na  ni  batili  na ni  lazima  ubadilishwe," mswada  huo  umesema.
 Wanadiplomasia  wanasema  wanatarajia  Marekani  kutumia  uwezo wake  wa  kura  ya turufu  kuzuwia  hatua  hiyo  wakati , wengi  kama  sio  wote , wajumbe  14  wa  baraza  la Usalama  wanatarajia  kuunga  mkono  mswada  huo  wa  azimio. (DW SWAHILI)

0 comments: