Sunday 24 December 2017

Idadi ya vifo yaongezeka Ufilipino katika kimbunga Tembin

Idadi ya waliofariki kufuatia kimbunga kilichopiga kusini mwa Ufilipino imefikia watu 182 mapema leo asubuhi, huku watu 153 wakiwa bado hawajulikani walipo. Kimbunga Tembin kimekuwa kikivuma katika kisiwa cha pili kwa ukubwa nchini humo cha Mindanao tokea Ijumaa iliyopita, na kusababisha mafuriko pamoja na maporomoko ya matope. Hapo jana maafisa wa polisi, wanajeshi na wafanyakazi wa kujitolea walilazimika kuchimba matope na vifusi kutafuta miili ya watu walioathirika katika kijiji cha Dalama. Wakati huo huo waokoaji waliopoa maiti kadhaa kutoka katika mto wa Salog karibu na mji wa Sapad. Idadi ya vifo katika rasi ya Zamboanga ya kisiwa cha Mindano pia imeongezeka hadi watu 28, na polisi imeripoti kwamba watu wengine 81 bado hawajulikani walipo baada ya matope na mawe kuporomoka katika jamii za pwani huko Sibuco na miji mingine ya uvuvi. Viongozi wa Ufilipino wamesema hapo jana kwamba maporomoko ya ardhi yamezuia misafara yauokoaji na misaada za kiutu kuyafikia maeneo masikini.

(DW SWAHILI)

0 comments: