Friday 5 January 2018

Watu 37 wafariki kutokana na mafuriko DRC

Watu zaidi ya 37 wamefariki baada ya mafuriko kuukumba mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Kinshasa kufuatia mvua kubwa, maafisa wa serikali wamesema.

Wengi wa waliouawa ni wakazi wa mitaa ya mabanda ambapo nyumba nyingi zimeharibiwa na maji ya mafuriko na maporomo ya ardhi.

Wengi kati ya wakazi milioni kumi wa mji wa Kinshasa huishi katika makazi duni katika maeneo tambarare na miundo mbinu ya kuondoa maji taka ni duni.
Waziri wa jimbo anayeangazia masuala ya kiafya na kijamii Dominique Weloli, alisema wengi wa waliofariki ambao ni pamoja na "watoto wawili au watatu waliokufa maji" walikuwa wanaishi Ngaliema, mtaa duni ambao umeathirika sana.

"Kumetokea si tu mafuriko bali pia maporomoko ya ardhi na nyumba kadha zimebomoka," Weloli amesema.
Kumekuwa na matukio ya vifo vinavyotokana na mafuriko karibu kila mwaka msimu wa mvua kubwa.

0 comments: