Monday 26 March 2018

Mo Salah kuongezewa mkataba Liverpool
Uongozi wa klabu ya Liverpool upo kwenye mipango ya kumuongezea mkataba mwingine Mshambuliaji wake kutoka Misri, Mohamed Salah.

Taarifa zinaeleza kuwa Liverpool itakuwa inamlipa mchezaji huyo kasi cha paundi £200,000 kwa wiki na kuzima ndoto za Real Madrid kumpata nyota huyo.

Salah amesema anafurahia zaidi kuchezea soka lake katika Ligi ya England sababu inaendana na aina ya uchezaji wake.

"Naipenda EPL sababu inaendana na aina ya uchezaji wangu, napenda kucheza hapa" alisema.

Real Madrid inatajwa kuwa klabu iliyoweka nguvu nyingi za kumsajili nyota huyo ambaye anafanya vizuri kwenye msimu huu wa ligi akiwa na Liverpool.
Wanafunzi Vyuo Vikuu Watajwa Kuongoza kwa Matusi Mitandaoni
Serikali imesema wanafunzi wa vyuo vikuu wanaongoza  kutukana na kutumia lugha zisizo na maadili kwenye mitandao ya kijamii.

Angalizo hilo limetolewa na naibu waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha  Jumamosi Machi 24, 2018 katika hafla fupi ya uzinduzi wa Unilife Compus iliyopo Mkoa wa Kilimanjaro uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Mwenge na kuvikutanisha vyuo vikuu vyote vya mkoa huo.

Alisema  yapo mambo matatu ambayo yanachangia wanafunzi kutofanya vizuri, yakiwamo matumizi mabaya ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama), anasa na starehe zilizopitiliza na kujiingiza kwenye siasa ambazo zinawanyima fursa ya kusoma vizuri.

“Serikali imebaini mambo yanayochangia kufifisha na kudidimiza jitihada za elimu tunayoitoa kuonekana bure. Kuna vitu ambavyo siyo vizuri  vinaendelea katika vyuo vyetu, ndizo changamoto tunatakiwa kukabiliana nazo. Chuoni unaweza kutengeneza au kuharibu maisha yako,” alisema.

Naye mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira alisema  wanafunzi wengi hawataki kujifunza  kwa kutumia muda vizuri kwa kusoma vitabu.

"Tunabaki kuwa waigaji wa dhana za wenzetu wa magharibi, hatutaki kujifunza vitu vipya bali vilevile vya wenzetu vinatumika hadi leo. Wasomi wa Tanzania tunajishusha kwa sababu ya kushindwa kuleta mawazo mapya kwenye sekta ya elimu na afya," alisema  Mghwira.
Watu 17 Watambuliwa Kati Ya 26 Waliofariki Katika Ajali Mkuranga
WATU 17 kati ya 26 waliofariki dunia katika ajali ya barabarani iliyotokea Mkuranga Mkoani Pwani ,wametambuliwa majina yao ambapo hatua inayoendelea ni kuwakabidhi kwa ndugu zao kwa ajili ya mazishi.

Aidha watu wengine kumi wamejeruhiwa na wamekimbizwa hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu.

Ajali hiyo imehusisha  gari  ndogo ya abiria aina ya Toyota Hiace yenye namba za usajili T.676 DGK inayofanya safari zake Kimanzichana – Mbagala Rangi na gari nyingine aina ya Lori.

Mganga mkuu wa hospitali ya wilaya ya Mkuranga, Stephen Mwandambo alisema amepokea maiti 25 na majeruhi hao ambapo majeruhi mmoja alifariki njiani wakati wakipelekwa hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Mganga mkuu huyo aliwataja waliofariki na kutambuliwa majina yao ni 17 kati ya 26 waliofariki kuwa ni pamoja na  Selemani Guli (36) mkazi wa Kongowe,Modesta Sheleli (24 ) mkazi wa Vianzi,Doreen Selemani Seleli (5), sheila Hamad Mkuba ( 8 )mkazi wa Vianzi na Mariam Hussein Sadik (15 )mkazi wa Mwarusembe.

“Nassoro Hamis( 48) mkazi wa Jaribu Mpaka, Asha Athumani (24)mkazi wa Songosongo ,Nasma Athuman 22 Songosongo Mwanahawa Athuman (52),Mohammed Saidi (25) mkazi wa Njopeka na Mwajabu Jongo (20)mkazi wa Njopeka”;

Dokta Mwandambo aliwataja wengine ni Mwarami Mbunju(37) mkazi wa Mkamba na Abisaalom Uloga (25)mkazi wa Kimanzichana ,Kijongo Kibwana Jongo(26 )anakaa Jaribu Mpakani na Recho Japhet (16),Mariam Selemani (36)mkazi wa Mbagala  na Melania Kapatwa (38)mkazi wa Jaribu Mpakani.

Inasemekana majeruhi waliopelekwa katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili wengine wamekatika viongo mbalimbali vya mwili.

Aidha dokta Mwandambo alisema wanakabiliwa na changamoto ya kipimo cha X-ray hali inayosababisha kushindwa kuwafanyia uchunguzi majeruhi .

Changamoto nyingine inayowakabili ni chumba cha kuhifadhia maiti kuwa kidogo kwani kina uwezo wa kuhifadhi maiti sita hivyo maiti 26 zipo nje ya uwezo wao.

Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia machi 25 mwaka huu katika eneo la Kitonga kata ya Mwalusembe wilaya ya humo.
Chanzo cha ajali inadaiwa mwendo kasi wa dereva wa lori katika kilima na kusababisha ajali hiyo mbaya.

Simanzi zimetawala katika wilaya hiyo ,ambapo mbunge wa jimbo la Mkuranga, Abdallah Ulega ,aliishukuru serikali ya wilaya chini ya mkuu wa wilaya ya Mkuranga Filberto Sanga kwa juhudi zake za kusaidia majeruhi na marehemu kupelekwa hospitalini .

Ulega alitoa pole kwa wafiwa na majeruhi na kuwaasa madereva waache kuendesha kwa mwendo kasi kwani husababisha ajali zembe.

“Naishukuru pia hospitali ya wilaya kwa juhudi zao baada ya kupokea marehemu na majeruhi kuhangaikia kuokoa maisha yao.” alieleza Ulega.
Watu 37 wafariki katika mkasa wa moto jumba la Kemerovo, Urusi
Watu 37 wamethibitishwa kufariki baada ya moto kuzuka katika jumba moja kubwa la kibiashara katika mji maarufu kwa uchimbaji wa mkaa wa mawe wa Kemerovo, eneo la Siberia nchini urusi.

Watu zaidi ya 64 hawajulikani walipo, wakiwemo watoto 41.

Baadhi ya maeneo ya jumba hilo kubwa yanadaiwa kuwa kwenye hatari ya kuporomoka.

Moto huo ulianza katika ghorofa ya juu katika jumba Winter Cherry.

Inadaiwa wengi wa waliofariki walikuwa kwenye kumbi za sinema.

Video zilizopakiwa mitandao ya kijamii zinawaonesha watu wakiruka nje kupitia madirisha kujaribu kujinusuru kutoka kwa moto huo uliozuka Jumapili.

Wazima moto zaidi ya 660 wametumwa kusaidia juhudi za uokoaji.

Chanzo cha moto huo hakijabainika lakini maafisa wameanzisha uchunguzi.

Kemerovo, ni eneo maarufu sana kwa uchimbaji wa mkaa wa mawe.

Ni mji unaopatikana takriban kilomita 3,600 mashariki mwa mji mkuu Moscow.

Kansela wa Austria Sebastian Kurz ametuma salamu zake za rambirambi kwa jamaa na marafiki wa waathiriwa, sawa na Waziri wa mambo ya nje wa Latvia Edgars Rinkēvičs.
 

Sunday 25 March 2018

Mamilioni waandamana kutaka udhibiti wa bunduki Marekani
Mamilioni ya watu waliandamana katika miji mbalimbali ulimwenguni kote siku ya Jumamosi kushinikiza mageuzi katika sheria zinzohusu umiliki wa bunduki.

Kilele cha maandamano hayo yaliyopewa jina la March for our lives, ulikuwa ni mkutano uliohudhuriwa na takriban watu nusu milioni katika mji mkuu wa Marekani, Washington DC.

Maandamano hayo yalipangwa na shule ya upili ya Marjorie Stoneman Douglas mjini Parkland, jimbo la Florida, ambako watu wapatao 17, wakiwemo wanafunzi 14 walipoteza maisha yao kufuatia shambulizi la bunduki kwenye shule hiyo mapema mwaka huu.

Zaidi ya maandamano 800 yalikuwa yamepangwa kufanyika katika miji kadhaa ya Marekani na sehemu nyingine duniani kote, sambamba na yale ya mjini Washington DC.

Mashambulizi ya kutumia bunduki zenye nguvu, hususan kwenye shule Marekani yamezua mjadala mkali, huku wanasiasa wakitofautiana kuhusu hatua za kudhibiti matukio hayo.

Wanaharakati na wasanii maarufu walihudhuria maandamano hayo, wakiwemo wanamuziki Jennifer Hudson, Ariana Grande, Demi Lovato na Miley Cyrus.

Mjukuu wa mtetezi maarufu wa haki za binadamu Martin Luther King Jr, alishangiliwa kwa shangwe na vigelegele aliposimama kuhutubia mkutano wa Washington. Yolanda Renee King III alisema kizazi cha sasa ndicho kitaleta mabadiliko yanayohitajika.

"Na itoshe! Na itoshe!" alisema msichana huyo.

Kundi kubwa la waandamanaji baadaye lilionekana nje ya ikulu likibeba mabango licha ya kuwa rais Donald Trump hakuwemo wakati huo. Baadaye waliyaweka mabango yao chini na kuyaacha nje ya uzio wa ikulu kama ishara kwamba walitaka rais Trump asome ujumbe wao.

Friday 23 March 2018